Halloween party ideas 2015
Image

·      Wajawazito walilia zahanati, watishia `kumwaga’ razi
Na Odriani Nicolaus, TSJ.

WAKAZI wa mtaa wa Mgeule, Kata ya Buyuni, Manispaa ya Ilala nje kidogo ya Jiji La Dar es Salaam, wameiomba halmashauri ya Manispaa hiyo kujenga daraja litakalounganisha eneo hilo na maeneo mengine ya jiji ili kuwa na uhakika wa mawasiliano kwao wakati wa mvua.
Mjumbe wa kamati ya Maendeleo ya Mtaa huo, Maliki Shemtandulo , (mwenye shati la kijani) akiwa na waandishi wa habari wa taasisi ya Wabunifumedia katika kutembelea mradi wa eneo linalotarajiwa kuwa Zahanati ya mtaa wa mgeule hivi karibuni (PICHA ETHAN MBUYA).


 Wakizungumza na timu ya waandishi wa habari waliotembelea miradi ya maendeleo katika maeneo ya pembezoni mwa Manispaa ya Ilala, walisema kukosekana kwa daraja hilo imekuwa chanzo cha maendeleo duni ya uchumi kutokana shughuli za kibiashara kukwama.

Mmoja wakazi hao  Bruno Benard Ndege alisema pia  kadhia hiyo  imechangia kushuka kwa kiwango cha elimu kutokana na wanafunzi wengi wa mtaa huo na ule wa Mgeule Juu kushindwa kwenda shule karibu kipindi chote cha msimu wa mvua.

“Tunashukuru juhudi za viongozi wetu wa mtaa, wamekuwa wakifanya kila njia kuondoa tatizo hili, lakini lazima kuwapo kwa suluhisho la kudumu kutoka serikalini hasa katika bajeti  ya Manispaa,”alisema Ndege.
Mjumbe wa shina na katibu wa mipango, fedha na uchumi,Bruno Benard Ndege, akiongozana na waandishi wa habari wa taasisi ya Wabunifumedia wakati wa kutembelea miradi ya maendeleo katika mtaa wa Mgeule hivi karibuni (PICHA ETHAN MBUYA). 
Ndege ambaye pia ni mjumbe wa shina katika eneo hilo, aliongeza kwa kusema kuwa ujenzi wa daraja hilo ni jambo mtambuka kutokana na matumizi ya barabara kuu ya kutoka eneo la Kwa Mbiki hadi Mgeule juu kutumiwa na zaidi ya mtaa mmoja katika shughuli za maendeleo na kibinadamu.

Mkazi mwingine,  Nurdin Shemtanduloo  alisema kutokuwepo kwa daraja hilo kunaweza kuathiri mpango wa serikali ya mtaa huo wa ujenzi wa soko kutokana na ukweli kwamba wafanyabishara wengi watashidwa kusafirisha bidhaa zao.
“Ujenzi wa daraja hili utasaidia kwenda na kasi ya sasa wa kufanya kazi kwa bidii, biashara na shughuli nyingine kama hizo za kupunguza au kumaliza kabisa umasikini,”alisema.

Mjumbe wa baraza la ardhi kata ya buyuni, mtaa wa mgeule, Elizabeth Mwakapangala, akizungumza na mkuu wa kitengo cha habari na mawasiliano kutoka WM, Yusuph Mwamba baaya ya taasisi hiyo ya habari kutembelea miradi ya maendeleo katika mtaa huo wa mgeule hivi karibuni (PICHA ETHAN MBUYA).
Naye Elizabeth Mwakapangala, alisema wanawake wengi wajawazito wamekuwa kwenye hatari zaidi wakati wa msimu wa mvua kutokana na kushindwa kufika hospitali ya wilaya ya Ilala, Amana,  kwa ajili ya kujifungua au zahanati ya Buyuni kushiriki kliniki.
 
“Wakati wa msimu wa mvua hali ya mama wajazito tunakuwa kwenye hatari zaidi kwasababu hakuna njia ya kupita, huweza kuwalazimu wanawake wengi kujifungulia nyumbani jambo ambalo ni hatari sana kwa afya ya mama na mtoto”alisema.
Zaidi, aliongeza kuwa ipo haja ya kuharakishwa kwa mchakato wa ujenzi wa zahanati kwenye mtaa huo na kuiomba serikali kusaidia juhudi za viongozi wa mtaa wao katika mpango wa kujenga zahanati ili kupunguza vifo vya mama na watoto ambao kwasbabu za kibiolojia kundi la mama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano hufa zaidi kwa ugonjwa wa malaria na matatizo ya uzazi.

Kuna watu wanaozuia huu mpango na eneo letu la zahanati, wajawazito na wanawake wengine tumeapa ipo siku tutawalaani hadharani na hakika tutamwaga razi mbele yao ili waone tumechoka na kero hii ya kukosa zahanati na maumivu ya uchungu hadi Amana au Buyuni,” alikasirika Mwakapangala.
Mjumbe wa kamati ya Maendeleo ya Mtaa huo, Maliki Shemtandulo alisema uongozi wa mtaa umewasilisha kero hiyo kwenye mamlaka serikali ingawa michango na juhudi za wananchi ni muhimu kufanikisha kero mbalimbali za mtaa huo.

Mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Mgeule, John Lazaro Mwatebela alisema kero ya daraja imewasilishwa kwa Mhandisi wa Manispaa ya Ilala na ameahidi kuingiza katika bajeti ya Manispaa katika mwaka huu wa fedha.

“Juhudi zetu kama jamii kwa sasa  ni kupunguza upana wa mto kwa kujaza kifusi ili kurahisisha  ujenzi huo mara utakapoanza ambapo, katika mazungumzo yetu na mhandisi alituahidi kwamba kabla ya Julai mwaka huu wataanza ujenzi baada ya upembuzi yakinifu kukamilika,”alisema.
Mtaa wa Mgeule ni mojawapo ya mitaa nane ya Kata ya Buyuni inayokabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo, maji safi, soko, umeme, zahanati na uhaba wa walimu katika shule mpya ya msingi Mgeule yenye walimu 14 wanaohudumia wanafuzi zaidi 700.

Kwa mujibu wa sera ya elimu ya mwaka 2003, mwalimu mmoja anatakiwa kuhudumia wanafunzi 45 katika chumba kimoja cha darasa  hivyo kufanya shule hiyo kwa sasa kuwa na hitaji la walimu 16 sawa na hitaji la walimu wawili zaidi.
JIUNGE NASI , BONYEZA HAPA http://www.wabunifumedia.blogspot.com ku-install App ya wabunifumedia,  bila ya kuingia website
Tweet@wabunifumediaonline, youtube@wabunifumediaonline TV, Fb@wabunifumediaonline, insta@wabunifumediaonline
 

Post a Comment

Theme images by Maliketh. Powered by Blogger.